Wednesday, May 2, 2012

SERIKALI YATAKIWA KUACHA KUINGILIAKAZI ZA TUME YA KATIBA


SERIKALI imetakiwa kuacha kuiingilia kazi za Tume ya Mabadiliko ya Katiba na badala yake iwape uhuru wa kufanyakazi hiyo kwa ufasaha na kuandaa katiba wanayoitaka wananchi.

Hayo yamesemwa jana na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Joseph Sinde Warioba wakati wa uzinduzi wa tume hiyo na kukabidhiwa jengo la kufanyia kazi hiyo.

Mwenyekiti huyo amesema isije ikafika wakati tume ikashindwa kufanyakazi ipasavyo kwa sababu ya maslahi ya watu wachache kwani kufanya hivyo itakuwa ni kuingilia uhuru wa tume na kuwanyima haki wananchi ya kupendekeza katiba waipendayo.

“ Nyie mliotuchagua tunaomba tafadhari mtupe nafasi isije ikaja leo au kesho mnaanza kutusumbua tupindishe kilichopo kwa madai mna watu wenu ndani ya tume naomba ieleweke kuwa tume si ya kikundi fulani ni ya wananchi  hivyo hatutaki kufanyakazi kwa presha ya watu fulani,”amesema Warioba.

Amesema kazi waliyopewa ni ngumu hivyo wana imani serikali itawapa ushirikiano wa kuwafikia wananchi wote ili waweze kutoa maamuzi yao na kuandaa katiba yenye maslahi ya umma.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue amesema Serikali imeandaa mazingira safi ya kuhakikisha tume hiyo inafanyakazi kwa ufanisi zaidi.

Amesema  kuwa serikali imetekeleza ahadi aliyoitoa rais alipoiapisha tume hiyo Aprili 13 mwaka huu ya kuhakikisha tume hiyo inafanyakazi kwenye mazingira stahiki yenye ulinzi wa kutosha, usalama , na vifaa vya mawasiliano na vya kutunzia kumbukumbu vya kisasa.

Pia serikali imenunua magari 30, kwa ajili ya tume hiyo ili kuweza kuwafikia wananchi kwa urahisi na kuepuka vikwazo katika utendaji wa kazi hiyo na fungu maalum la fedha limetengwa..

“ Serikali imedhamiria kuipa uhuru tume, kuwapa sehemu nzuri ya kufanyiakazi pamoja na nyumba za kuishi wana tume ambao wanatoka nje ya Dar es Salaam,”amesema Sefue.

Naye Waziri wa Katiba na Sheria, Cellina Kombani  amesema umuhimu wa mabadiliko ya katiba ya nchi ni mkubwa na wananchi wana matumaini na tume na ndiyo maana ilipotangazwa hakuna malalamiko yaliyojitokeza.

Ameitaka tume hiyo ijipange vyema ili kuhakikisha inatoa elimu ya katiba iliyopo ili wananchi waweze kutoa maoni ya katiba waipendayo kwani muundo wa katiba hiyo ni jambo nyeti na lenye kuleta msisimuko.

“ Nina imani amani  itatawala na uwazi, kwani mchakato huu ni wa kuboreha mazuri, kuondoa mapungufu pia ni kujipima tulikotoka na tuendako kwani nia si kuvunja umoja wetu bali mawazo ya wananchi yataheshimiwa, “amesema Kombani.

Kombani ameongeza kuwa tume hiyo ndiyo nguzo ya mchakato wa katiba mpya huku akisisitiza kufanikiwa au kutofanikiwa kutatokana na tume hiyo kutekeleza majukumu yao kwa kuwashirikisha wananchi bila ubaguzi.

“ Kazi hii inahitaji ushirikiano zaidi nafahamu kuna kipindi mtakwazika na kutamani kuimbia kazi hii lakini mkiwashirikisha wananchi mtafikia muafaka na hatimaye tutapata katiba inayostahili,”amesema Kombani.


Wakati huohuo, Waziri wa Katiba na Sheria Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Abubakari Khamis Bakari amesema tume imepewa kazi ngumu ya kuwaelimisha wananchi kwani wengi wao hawajui maana ya muungano.

Amesema ili katiba iwe yenye kukidhi haja ni muhimu wananchi wakapewa fursa ya kutoa maoni ambayo yataisaidia tume hiyo  kurahisisha kazi yao.


Amewatahadharisha wananchi kuacha kutumia mchakato huo kama njia ya kuibomoa nchi  na badala yake fursa hiyo itumike kuunda katiba yenye mantiki na inayokubaliwa na watu wote.

Hata hivyo hafla hiyo iliingiliwa na dosari baada ya jenereta lililopo jirani na jengo hilo kulipuka jana asubuhi na kusababisha umeme katika jengo hilo kukatika  hivyo kufanya hafla hiyo kuendeshwa bila vipaza sauti.

mwisho

No comments:

Post a Comment