Monday, April 29, 2013


Brandts aisoma Simba dakika 45
*Asema hawana kitu, ni warahisi sana watakiona Mei 18
*Ashangaa Yanga walifungwaje 5-0, awatoa hofu mashabiki
Na Humphrey Shao, Dar es Salaam

DAKIKA 45 zilitosha kumuondoa uwanjani Kocha wa Yanga, Ernest Brandts, baada ya kuona zinatosha kuisoma timu ya Simba pindi ilipokuwa ikicheza na Polisi Morogoro, katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara iliyochezwa juzi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Brandts ambaye aliwasili katika mchezo huo  dakika kumi kabla ya mchezo kuanza, akiongozana na mmoja wa watumishi wa klabu hiyo na kuketi jukwaa kuu, alikuwa ameshika ‘notebook’ akiandika kila  kinachojiri katika mchezo huo.
Kocha huyo alipata nafasi ya kushuhudia ni jinsi gani Simba ikicheza, hadi kuona namna walivyoweza kufanya makosa na kupachikwa bao la mapema kabla ya kusawazisha, lakini aliondoka baada ya kumalizika kipindi cha kwanza, ili aweze kuendelea na majukumu mengine.
MTANZANIA ilifanya jitihada na hatimaye kupata nafasi kuzungumza na kocha huyo, akiwa ndani ya gari yake aina ya Prado wakati akijiandaa kuondoka uwanjani hapo, na kumuuliza kwanini anaondoka mapema uwanjani na kujibu tayari amekipata alichokuwa anakitaka kutoka kwa wapinzani wake.
“Sioni sababu ya kuendelea kukaa hapa wakati kazi iliyonileta hapa nimemaliza, naendelea na programu nyingine kwani nimewaona Simba wakicheza na kwangu sio tishio wanacheza rahisi sana kuliko nilivyofikiri na wachezaji wangu, naamini nitawafunga tu.
 “Nakumbuka mara ya kwanza nilipopewa majukumu ya kuinoa timu hii, nilipewa habari za wapinzani wetu kutufunga bao 5-0 msimu uliyopita, sikuliweka akilini kwakuwa nilikuwa nataka timu ifanye vizuri kwanza na imekuwa hivyo, sasa tutakutana Mei 18,” alisema Brandts.
Mholanzi huyo alisema, Simba wamepoteza kiwango kabisa, hata wale wachezaji vijana ambao wamepewa nafasi katika timu hiyo, bado hawajaizoea ligi vizuri, hivyo udhaifu huo utaisadia timu yake kushinda katika mechi hiyo.
Alisema kikosi chake kimeimarika, wachezaji wake hawatacheza kwa presha kwani tayari kombe wanalo, wanachotakiwa kufanya ni kurudisha heshima ambayo waliipoteza, ambapo walifungwa na kunyang’anywa kombe.

“Nimewaona Simba nitakwenda kufanyia kazi mapungufu yao, ambayo yamejitokeza ili kuweza kuimarisha kikosi kiweze kuwasambaratisha Simba ipasavyo, mashabiki wategemee ushindi hakuna tena 5-0,” alisema.
Aliongeza kikosi chake kipo tayari kwa ajili ya kuivaa Coastal Union kesho na kuondoka na pointi tatu muhimu, licha ya timu yake kutangazwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania bara, hivyo hakutakuwa na kigezo cha kupoteza mechi hata moja kati ya hizo zilizosalia.

No comments:

Post a Comment